Friday, May 10, 2013

USIFE KWANZA MPENZI WANGU - 5



ILIPOISHIA...
Mkakati wa kwanza wa Levina, ulikuwa ni kumchonganisha Rashid na mama yake. Akili yake ikafanya kazi kama umeme. Kitu pekee ambacho kingeweza kuwafanya mama yake amchukie Rashid ni kama angemwambia kuwa alikuwa akimsumbua kimapenzi.
“Yap, lazima nifanye hivyo,” akawaza Levina.
Ilikuwa lazima afanye hivyo, hata hivyo halikuwa zoezi gumu kwake, maana tayari alikuwa ameshajitumia meseji kwenye simu yake kupitia simu ya Rashid. Alikuwa amebakiza kazi ndogo sana.
SASA ENDELEA...

JIONI moja alipokuwa akikazitiza sebuleni wakati ametoka kazini, alimwona mama yake akiwa amekaa kimya, akili yake ikiwa kwenye runinga aliyokuwa akiangalia. Akamrushia mama yake simu yake...
“Mama hebu soma hii meseji,” Levina alimwambia mama yake akiwa amesimama wima, uso wake akiwa ameukunja sana.
“Una nini?”
“We soma tu!”
“Hata salamu!”
“Nimeshachanganyikiwa kabisa mama....shikamoo!”
“Mar-haba, haya ni meseji ya nani?”
“Soma kwanza mama, nitakuambia ni kwanini nimekuletea.”
Mama Levina akachukua ile simu iliyokuwa mapajani mwake na kusoma ile meseji iliyokuwa ikionekana kwenye kioo cha simu. Mama Levina hakuamini macho yake, maneno aliyokutana nayo kwenye kioo cha simu, yalimchanganya sana.
Hakuamini!
“Nani amekutumia?”
“Rashid mama,” Levina akasema akionekana mwenye uso wenye huzuni sana.
“Nini?” Mama Levina akauliza tena akiwa ameonekana kukasirika zaidi.
“Ni Rashid mama, tena nimevumilia kwa muda mrefu lakini haachi kunitumia meseji zake za kijinga, mbaya zaidi nimeshamuonya lakini wapi!”
“Ameanza lini huu mchezo?”
“Jumapili mama, wakati nyie mmeenda kanisani, yeye akaanza kuniambia mambo yake ya ajabu!”
“Pumbavu kabisa...” mama Levina akasema kisha akaanza kumuita kwa sauti kubwa...
“Rashidiiiiii...Rashidiiiiii...Rashidiiiiiii...” mama yake akaita kwa sauti ya juu kwa ukali kidogo.
“Naam mama!”
“Njoo haraka sana.”
“Nakuja mama.”
Rashid alivyofika tu, mama Levina akamtupia simu...
“Soma kwa sauti hiyo meseji!” Mama Levina akasema kwa hasira.
“Meseji gani mama?”
“Unajifanya hujui siyo?”
“Meseji ipi?”
“Hiyo inayoonekana hapo kwenye simu.”
Muda wote Levina alikuwa kimya akimwangalia Rashid anavyobabaika, kwa ndani alianza kumuonea huruma lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa lazima amuonee ili dhamira yake iweze kutimia.
Maneno yaliyokuwa kwenye ile meseji yalikuwa mazito sana kutamkika mbele ya mama Levina, lakini alijua kabisa kwamba yeye hakutuma ule ujumbe.
Meseji yenyewe ilisomeka: “Samahani kwa ujumbe huu, lakini sasa nataka kutua huu mzigo mzito uliopo ndani ya moyo wangu. Nakupenda sana Levina, naomba ukubali ombi langu!”
Rashid alishtuka sana, akashindwa kujua namna ambavyo angeweza kujitetea.
“Mama sijatuma hiyo meseji mimi!”
“Funga mdomo wako.”
“Mama huyu Rashid alishaanza huu mchezo wake muda mrefu sana, wakati mwingine nikipita ananikonyeza, yaani anaonekana amekosa kabisa heshima. Yaani Rashid unataka kutembea na mimi kweli?” Levina akasema akitengeneza hasira.
“Dada mwogope Mungu, lini nimekutumia hiyo meseji!” Rashid akasema akianza kulia.
“Hebu simu yako!” Mama Levina akasema.
Rashid akampa mama Levina simu, akaenda moja kwa moja hadi kwenye Messages kisha akaingia kwenye Sent Items, akakutana na meseji nyingi ambazo zimetoka kwenye simu ya Rashid kwenda kwenye simu ya Levina.
“Acha kulia unafiki hapa...hii nyumba si danguro na sihitaji maneno zaidi na wewe, ninachokuomba chukua kila kilicho chako, halafu nikulipe pesa zako uondoke kwangu!”
“Mama naonewa mama, sijafanya hivyo na wala siwezi kufanya ujinga kama huo mama!”
“Kwahiyo mwanangu anakusingizia?”
“Na sijui ni kwanini ameamua kufanya hivyo!”
“Rashid sasa naona unataka kunigombanisha na familia yangu, tafadhali chukua kila kilicho chako uje nikulipe vipesa vyako uondoke kwangu, sina lingine!” Mama Levina akasema kwa kumaanisha.
Rashid akaondoka na kwenda chumbani mwake kukusanya mizigo yake akiwa analia. Levina akabaki na mama yake sebuleni, moyoni Levina aliumia sana, lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa lazima Rashid aondoke ili amwingize Deo ambaye alitamani sana baadaye awe mumewe.
Mama Levina hakujua kilichoendelea kabisa. Ilibaki kuwa siri ya Levina peke yake.
Levina aliumia ndani kwa ndani, alikiri kabisa kwamba Rashid hakuwa anahusika na chochote katika mchezo ule. Kitu pekee kilichomsukuma kufanya vile ni mapenzi yake ya dhati pekee, hakuwa na kitu kingine ndani yake zaidi ya hivyo.
Tangu Rashid alipoondoka kwenda chumbani kwake kukusanya mizigo yake, alijisikia mkosaji sana.
Mwenye roho mbaya sana!
Alijihisi kama si binadamu kabisa!
Sifa zote mbaya akajipa yeye!
Mama yake aliweza kugundua tofauti aliyokuwa nayo mwanaye, akaona njia pekee ya kugundua kilichokuwa kikimtatiza mwanaye ni kumuuliza tu!
“Nini tatizo tena mwanangu?”
Levina akabaki kimya!
“Levina...” mama yake akaita.
“Abee...” Levina akaitikia kwa kushtuka kidogo.
Ni kama alikuwa amegutuka kutoka katika usingizi mzito, lakini ukweli haukuwa huo. Levina alikuwa na mawazo ya usaliti. Kusema uongo na kumnyanyasa Rashid kwasababu ya mapenzi.
“Una nini mama?!!”
“Inaniuma sana mama...” Levina akasema machozi yakidondoka machoni mwake, ni kama alikuwa akiumizwa na meseji za Rashid, lakini ukweli halisi haukuwa huo.
Ndani ya nafsi yake alikuwa akiumizwa na kitendo cha kumsingizia na si kufanyiwa kama ambavyo alitaka kutengeneza.
“Lakini ndiyo nimemtimua hivyo.”
“Amekosa adabu kabisa, yaani siku zote hizo naishi naye kama kaka yangu halafu anakuja kuniambia maneno machafu kiasi hicho? Hana adabu kabisa...” akasema Levina lakini kichwani mwake kukiwa na kitu kingine.
Moyoni mwake alihifadhi kitu tofauti kabisa, alikuwa na siri nzito sana, ambayo hakutakiwa kumwambia mtu yeyote, ilikuwa ni siri ambayo alitakiwa kuijua yeye na moyo wake pekee.
“Potelea mbali, kama ni kazi anaweza kupata mahali pengine, lakini nitapata wapi mwanaume kama Deo, lazima nifanye hivi, sina namna!” akazidi kuwaza kichani mwake.
“Usijali mwanangu, nimeshamtimua huyu mwanaharamu. Hutakiwi kuwa na mawazo mwanangu na mimi mama yako nipo. Tena subiri...wewe Rashid, unasubiri nini? Kwani una mizigo gani mingi ya kuchukua muda mrefu kiasi hicho?” akasema mama Levina akisimama kumfuata chumbani kwake.
Mama Levina alikuwa amevimba kwa hasira, akafika chumbani kwa Rashid na kumwita kwa sauti kubwa...
“Si naongea na wewe, hebu toka haraka nyumbani kwangu.”
“Natoka mama, lakini siku moja utakuja kugundua ukweli, siwezi kufanya mambo ya ujinga kiasi hicho mama,  kwakuwa wewe umeamua kumuamini Levina sawa!”
“Tena funga domo lako kabisa wewe mwanaharamu, inaonekana unataka kunigombanisha na mwanangu, unataka kuniambia mwanangu anaongopa?”
“Ndiyo mama!”
“Kwa lipi hasa?”
“Sijui mama, lakini ukichunguza utagundua ukweli.”
“Tena ishia hapo hapo kuniita mama, anayeruhusiwa kuniita mama ni yule anayeheshimu wanangu na kuwachukulia kama dada zake, si wewe mpumbavu!”
“Hapana mama!”
“We’ mwendawazimu, sina muda wa kubishana zaidi. Paki vitu vyako, nakwenda kukuchukulia pesa zako uondoke!”
Rashid akabaki kimya.
Mama Levina akaenda ndani haraka na kuchukua fedha alizokuwa akidaiwa na Rashid kisha akarudi na kumkuta tayari ameshajiandaa.
“Chukua pesa zako, tena nimekuongezea na elfu thelathini zikusaidie, ondoka kwangu!”
“Ahsante mama, lakini Mungu mwenyewe ndiye anayejua ukweli wa haya yote!”
“Hayo mahubiri yako huwa nakutana nayo kanisani, sasa sioni kama hata hapa nyumbani kwangu panafaa kuhubiriwa!”
“Siyo mahubiri mama, ni ukweli kabisa kutoka ndani ya moyo wangu!”
“Ukweli wa nini?”
“Sijamtumia zile meseji mimi mama.”
“Hivi wewe una akili? Zile namba ni zako au za nani?”
“Zangu.”
“Sasa kama ni zako, kwanini unaruka?”
“Unajua mama...juzi...” mama Levina hakumpa nafasi ya kumalizia utetezi wake.
“Hebu toka kwangu haraka tafadhali, sidhani kama bado nina nafasi ya kuendelea kuusikiliza utumbo wako, ondoka tafadhali!”
Rashid alikuwa anataka kumweleza mama Levina kwamba kuna siku alimuazima simu yake, lakini hakupewa nafasi hiyo. Rashid akaondoka analia, mama Levina akiendelea kufoka huku akirusha mikono.
Alikuwa amekasirika sana. Pamoja na utendaji kazi wake kuwa mzuri kwa muda mrefu aliokuwa akikaa naye, lakini siku aliyasahau yote hayo kwa meseji iliyoonekana kutumiwa mwanaye.
***
Mto wote ulikuwa umelowana kwa machozi, Levina alikuwa na uchungu sana ndani ya moyo wake. Usiku huo ulikuwa mgumu sana kwake, aliteswa na watu mawili; DEO na RASHID!
Alifanya dhambi ya kumsingizia Rashid kwamba amemtongoza na akafukuzwa kazi. Hilo lilimuuma, lakini lingepoa kama kweli Deo angekubali kuwa naye. Lakini aliteseka sana, akiwa hana uhakika kama kweli Deo atamkubalia.
Tabu yote ya nini? Usiku ule ule akachukua simu na kumpigia Deo.

Itaendelea...

Thursday, May 9, 2013

USIFE KWANZA MPENZI WANGU - 4



ILIPOISHIA...
Kama ni mateka, alikuwa mateka asiye na hali, ambaye pamoja na kutekwa kwenyewe, alikuwa tayari kufanywa mateka. Levina alijishangaa sana jinsi alivyotokea kumpenda Deo.
Hakika hakuwa hadhi ya mwanaume wa kuwa  naye, uwezo wao kifamilia, heshima waliyonayo wazazi wake ni kati ya mambo ambayo yalimchanganya sana na kumfanya ashindwe kuwa na maamuzi ya moja kwa moja ya nini cha kufanya kwa ajili ya Deo.
Pamoja na yote hayo, moyo wake ulikuwa na kitu kimoja tu...
Mapenzi!
SASA ENDELEA 

AALIMPENDA sana Deo, lakini alikuwa na changamoto nyingi sana kichwani mwake. Kwanza aliwaza juu ya wazazi wake...hakujua kama wangekubaliana na wazo lake la kuolewa na Deo, kijana fukara ambaye hana mbele wala nyuma.
Hilo lilimchanganya sana kichwa chake, lakini alijipa moyo kwamba siku moja lazima Deo angekuwa mikononi mwake, yeye akiwa mama na Deo akiwa baba.
“Hilo nitahakikisha nalitimiza, maadamu nimempenda, hayo mengine nitajua baadaye!” akawaza Levina.
***
“Mambo Deo?” alikuwa ni Levina akimsalimia Deo, asubuhi ya siku iliyofuata alipokwenda sokoni.
“Poa, za nyumbani?”
“Salama.”
“Kilo ngapi?”
“Hapana, leo sihitaji mchele, nimekuletea zawadi yako,” akasema Levina akimkabidhi bahasha ya khaki.
Deo akapokea...
“Hiyo ni simu Deo, imebidi nikununulie ili kurahisisha mawasiliano yetu.”
“Mh! Ahsante sana jamani, lakini kwanini umeamua kufanya hivi?”
“Kwasababu sisi ni marafiki, unajua tunatakiwa kudumisha urafiki wetu kwa kuwasiliana mara kwa mara, au wewe hupendi tukiwa marafiki?”
“Napenda sana, nashukuru sana!”
“Usijali, line imo humo humo ndani, tayari nimeshakuwekea vocha za elfu ishirini, zikiisha nijulishe nikuongeze nyingine.”
“Ahsante sana,” Deo akashukuru tena.
Haikuwa rahisi kuamini jambo hilo, zawadi ile kwa Deo ilikuwa zaidi ya zawadi, ule ulikuwa uthibitisho tosha kwamba Levina alikuwa anampenda.
Levina hakukaa muda mrefu sana, akaaga na kuondoka.
***
Siku zilivyozidi kwenda na kuwasiliana, mapenzi kati ya wawili hawa yalizidi kuchipuka kwa kasi, lakini si Deo wala Levina aliyekuwa tayari kueleza hisia zilizokuwa ndani ya moyo wake.
Wote waliishi na siri nzito za mapenzi ndani ya nafsi zao, lakini leo Levina amepata wazo la kufanya ili aweze kumnasa Deo. Alitumia kila njia kumuonesha kwamba anampenda na alichokuwa akikisibiri siku zote ni Deo kumtamkia kwamba anampenda, lakini hilo halikutokea.
Deo naye alishangazwa na jinsi Levina alivyopenda kuwa naye karibu na kumsaidia mambo mbalimbali, lakini aliogopa kumwambia kwamba anampenda, akihofia kupoteza urafiki wao ambao kwake ulikuwa na manufaa makubwa sana.
Levina ameshapata njia za kumsogeza karibu Deo ili iwe rahisi kwake kutamka kwamba anampenda. Alipanga mpango hatari, haukuwa mwingine zaidi ya kufanya jitihada mfanyakazi wao kwa kiume wa nyumbani atimuliwe ili amfanyie Deo mipango ya kupata kazi nyumbani kwao.
Hapo ndipo angempata Deo kwa urahisi zaidi, maana angekuwa anammiliki. Hilo alijihakikisha kulifanya.
***
Levina alikuwa mateka wa mapenzi, alimpenda sana Deo na alitaka kuhakikikisha anakuwa wake wa maisha yake yote. Kitu pekee kilichokuwa kichwani mwake ilikuwa ni namna gani angeweza kumwondoa Rashid nyumbani kwao na kufanya jitihada za kumwingiza haraka sana Deo nyumbani, hapo lengo lake lingeweza kutimia bila mushkeli kabisa.
“Mimi ndiye ninayejua thamani ya penzi langu kwa Deo, najua kama nikimwambia ghafla anaweza kunichukia na kuniona malaya, lakini nikimsogeza kwanza nyumbani, naamini itakuwa vyema zaidi maana hataweza kupindua,” akawaza kichwani mwake Levina.
“Lazima atakuwa wangu, lazima...” akazidi kujihakikishia ushindi.
Tayari alishakuwa na mbinu zake, mipango ilikuwa tayari kabisa, kilichobaki ilikuwa ni utekelezeji tu.
“Rashid hana ujanja wowote kwangu, mimi ndiye Levina na nitahakikisha namtoa nyumbani,” akazidi kupanga mipango ya kummaliza.
***
Ilikuwa Jumapili asubuhi, nyumba ikiwa kimya kabisa, wazazi wa Levina, mdogo wao mdogo pamoja na house girl wote walikuwa wamekwenda kanisani, nyumbani wakiwa wamebaki Levina na Rashid, kijana wa kazi.
“Rashidiiiiiii....” Levina akaita akiwa amekaa sebuleni akiangalia runinga.
“Naam dada...”
“Njoo!”
“Nakuja.”
Rashid akakimbia haraka hadi sebule alipokuwa akiitwa na Levina. Akamkuta akiwa ametulia kwenye sofa.
“Mambo kaka?” Rashid akasalimia.
“Poa, mzima?”
“Nipo poa, nina shida moja muhimu nataka unisaidie.”
“Nini?”
“Naomba uniazime simu yako mara moja, maana yangu imekufa display!”
“Haina pesa lakini.”
“Usijali, ninayo nitaongeza, kuna mtu nataka kuchat naye kidogo!”
“Hii hapa.”
“Poa basi, nikimaliza nitakushtua, unafanya nini nje?”
“Nakatia fensi, si unajua tena dingi akija akikuta sijakamilisha anaweza kuniletea muziki?”
“Poa bwana endelea.”
Levina akachukua ile simu na kuiangalia wa dharau...
“Nakumaliza na simu yako hii hii,” akawaza kichwani mwake Levina.
Zoezi kubwa lililokuwa likiendelea ni kutuma meseji kutoka kwenye simu ya Rashid kwenda kwenye simu yake, huku akijibizana naye. Alipomaliza, akafuta meseji zote zilizoingia na kutoka kwenye simu ya Rashid, ili kuondoa ushahidi.
Baadaye akamrudishia Rashid simu yake.
“Umefanikiwa kuwasiliana naye?” Rashid akamwuliza Levina.
“Siyo kuwasiliana naye, ni kuwasiliana nao?”
“Kwani walikuwa wangapi?”
“Nilikuwa nachat na marafiki zangu kibao, si mmoja kama unavyodhani.”
“Poa, mi nipo nje.”
“Sawa kaka Rashid.”
Kwa alivyokuwa akizungumza, ni kama muungwana mwenye roho nzuri na upendo, lakini kikubwa alikuwa amepanga kumfukuzisha kazi Rashid. Ni kijana aliyefanya kazi kwao kwa muda mrefu sana, akiaminiwa sana na wazazi wake, isingekuwa rahisi kumtoa nyumbani kwao kienyeji kutokana na utendaji wake kuwa bora kwa miaka mitatu aliyoishi kwa uaminifu mkubwa katika nyumba ile.
***
“Samahani kwa kukusumbua Deo, naamini wewe ni rafiki yangu, ni kweli?” Levina alimwambia Deo jioni moja alipomsubiri Magomeni - Mwembechai, ambapo Deo alikuwa anarudi nyumbani Mburahati.
“Naamini hivyo, sisi ni marafiki.”
“Kweli?”
“Naamini hivyo au?”
“Hata mimi pia, lakini nilitaka kupata uhakika kutoka kwako.”
“Sisi ni marafiki Levina.”
“Bila shaka huwezi kunificha chochote katika maisha yako.”
“Hilo halina ubishi.”
“Ulisema unaitwa Deo, ukoo wako ni nani na wewe ni kabila gani?”
“Mh! Jamani, kwanini?”
“Nataka tu, kujua.”
“Niite Deogratius Mgana, ni mwenyeji wa Kiomboi, Singida, nikimaanisha kwamba mimi ni Mnyiramba.”
“Ok! nimefurahi sana kukufahamu kwa uzuri Deo, mimi ni Levina Masamu, ni Mchagga wa Old Moshi, Kilimanjaro.”
“Oh! Ahsante sana kukufahamu zaidi, lakini kwanini umeniuliza yote hayo?”
“Nina maana yangu, utaijua baadaye kidogo. Samahani, mshahara wako ni shilingi ngapi kwa mwezi?”
“Nalipwa elfu arobaini na tano.”
“Jamani zinakutosha kweli?”
“Nitafanyaje Levina, maisha...”
“Elimu yako ni kiasi gani?”
“Mimi?”
“Ndiyo!”
“Darasa la saba tu, nilifaulu lakini wazazi wangu wakakosa fedha za kuniendeleza.”
“Usijali, vipi utakuwa tayari nikikitafutia mahali pengine utakapolipwa fedha nyingi zaidi?”
“Ndiyo, hata sasa hivi.”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
Levina akafurahi sana, mpango wake ulikuwa unanukia kukamilika.
Deo alikuwa akikubaliana na matakwa yake bila mwenyewe kujua. Ndani ya nafsi yake alikuwa na furaha isiyo na kifani. Alijisikia mshindi kwa kiasi kikubwa sana.
Levina akashindwa kuficha tabasamu lake mwanana usoni mwake, akalichanua na kuzidi kumwongea uzuri wake ambao haukuwa wa kujificha.
“Vipi, mbona umetabasamu?” Deo akauliza.
“Hapana, nafurahi jinsi ambavyo unaweza kujieleza. Unajua Deo, mimi napenda sana watu wakweli, kwangu ukishakuwa mkweli basi najisikia amani kabisa, ndiyo maana nacheka au nimekuudhi?”
“Kwasababu ya kutabasamu?”
“Labda!”
“Haitatokea Levina, tabasamu ni alama ya furaha, sasa ni nani ambaye anachukia furaha?”
“Basi umeshinda...lakini kuna jambo nataka kukuuliza.”
“Sawa.”
“Je, utakuwa tayari kusoma, kama nikiamua kukusaidia?”
“Jamani...tena hiyo ni ndoto yangu ya kila siku, nilikuwa naendelea kujichanga ili nipate pesa za kuanza masomo hata ya elimu ya watu wazima.”
“Vizuri sana, haya yote nitayafanyia kazi. Naona nikuache uwahi nyumbani, lala ukijua kwamba nayafanyia kazi mambo yote hayo. Mimi ni rafiki yako Deo, shaka ondoa.”
“Najua Levina, ahsante sana rafiki yangu mwema.”
“Poa.”
***
Mkakati wa kwanza wa Levina, ulikuwa ni kumchonganisha Rashid na mama yake. Akili yake ikafanya kazi kama umeme. Kitu pekee ambacho kingeweza kuwafanya mama yake amchukie Rashid ni kama angemwambia kuwa alikuwa akimsumbua kimapenzi.
“Yap, lazima nifanye hivyo,” akawaza Levina.
Ilikuwa lazima afanye hivyo, hata hivyo halikuwa zoezi gumu kwake, maana tayari alikuwa ameshajitumia meseji kwenye simu yake kupitia simu ya Rashid. Alikuwa amebakiza kazi ndogo sana.

Itaendelea...