ILIPOISHIA...
Mkakati wa kwanza wa Levina, ulikuwa ni kumchonganisha Rashid na mama yake.
Akili yake ikafanya kazi kama umeme. Kitu pekee ambacho kingeweza kuwafanya
mama yake amchukie Rashid ni kama angemwambia kuwa alikuwa akimsumbua
kimapenzi.
“Yap, lazima nifanye hivyo,” akawaza Levina.
Ilikuwa lazima afanye hivyo, hata hivyo halikuwa zoezi gumu kwake, maana
tayari alikuwa ameshajitumia meseji kwenye simu yake kupitia simu ya Rashid.
Alikuwa amebakiza kazi ndogo sana.
SASA ENDELEA...
JIONI moja alipokuwa akikazitiza sebuleni wakati ametoka kazini, alimwona
mama yake akiwa amekaa kimya, akili yake ikiwa kwenye runinga aliyokuwa
akiangalia. Akamrushia mama yake simu yake...
“Mama hebu soma hii meseji,” Levina alimwambia mama yake akiwa amesimama
wima, uso wake akiwa ameukunja sana.
“Una nini?”
“We soma tu!”
“Hata salamu!”
“Nimeshachanganyikiwa kabisa mama....shikamoo!”
“Mar-haba, haya ni meseji ya nani?”
“Soma kwanza mama, nitakuambia ni kwanini nimekuletea.”
Mama Levina akachukua ile simu iliyokuwa mapajani mwake na kusoma ile
meseji iliyokuwa ikionekana kwenye kioo cha simu. Mama Levina hakuamini macho
yake, maneno aliyokutana nayo kwenye kioo cha simu, yalimchanganya sana.
Hakuamini!
“Nani amekutumia?”
“Rashid mama,” Levina akasema akionekana mwenye uso wenye huzuni sana.
“Nini?” Mama Levina akauliza tena akiwa ameonekana kukasirika zaidi.
“Ni Rashid mama, tena nimevumilia kwa muda mrefu lakini haachi kunitumia
meseji zake za kijinga, mbaya zaidi nimeshamuonya lakini wapi!”
“Ameanza lini huu mchezo?”
“Jumapili mama, wakati nyie mmeenda kanisani, yeye akaanza kuniambia mambo
yake ya ajabu!”
“Pumbavu kabisa...” mama Levina akasema kisha akaanza kumuita kwa sauti
kubwa...
“Rashidiiiiii...Rashidiiiiii...Rashidiiiiiii...” mama yake akaita kwa sauti
ya juu kwa ukali kidogo.
“Naam mama!”
“Njoo haraka sana.”
“Nakuja mama.”
Rashid alivyofika tu, mama Levina akamtupia simu...
“Soma kwa sauti hiyo meseji!” Mama Levina akasema kwa hasira.
“Meseji gani mama?”
“Unajifanya hujui siyo?”
“Meseji ipi?”
“Hiyo inayoonekana hapo kwenye simu.”
Muda wote Levina alikuwa kimya akimwangalia Rashid anavyobabaika, kwa ndani
alianza kumuonea huruma lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa lazima amuonee ili
dhamira yake iweze kutimia.
Maneno yaliyokuwa kwenye ile meseji yalikuwa mazito sana kutamkika mbele ya
mama Levina, lakini alijua kabisa kwamba yeye hakutuma ule ujumbe.
Meseji yenyewe ilisomeka: “Samahani kwa ujumbe huu, lakini sasa nataka
kutua huu mzigo mzito uliopo ndani ya moyo wangu. Nakupenda sana Levina, naomba
ukubali ombi langu!”
Rashid alishtuka sana, akashindwa kujua namna ambavyo angeweza kujitetea.
“Mama sijatuma hiyo meseji mimi!”
“Funga mdomo wako.”
“Mama huyu Rashid alishaanza huu mchezo wake muda mrefu sana, wakati
mwingine nikipita ananikonyeza, yaani anaonekana amekosa kabisa heshima. Yaani
Rashid unataka kutembea na mimi kweli?” Levina akasema akitengeneza hasira.
“Dada mwogope Mungu, lini nimekutumia hiyo meseji!” Rashid akasema akianza
kulia.
“Hebu simu yako!” Mama Levina akasema.
Rashid akampa mama Levina simu, akaenda moja kwa moja hadi kwenye Messages
kisha akaingia kwenye Sent Items, akakutana na meseji nyingi ambazo zimetoka
kwenye simu ya Rashid kwenda kwenye simu ya Levina.
“Acha kulia unafiki hapa...hii nyumba si danguro na sihitaji maneno zaidi
na wewe, ninachokuomba chukua kila kilicho chako, halafu nikulipe pesa zako
uondoke kwangu!”
“Mama naonewa mama, sijafanya hivyo na wala siwezi kufanya ujinga kama huo
mama!”
“Kwahiyo mwanangu anakusingizia?”
“Na sijui ni kwanini ameamua kufanya hivyo!”
“Rashid sasa naona unataka kunigombanisha na familia yangu, tafadhali
chukua kila kilicho chako uje nikulipe vipesa vyako uondoke kwangu, sina
lingine!” Mama Levina akasema kwa kumaanisha.
Rashid akaondoka na kwenda chumbani mwake kukusanya mizigo yake akiwa
analia. Levina akabaki na mama yake sebuleni, moyoni Levina aliumia sana,
lakini hakuwa na jinsi, ilikuwa lazima Rashid aondoke ili amwingize Deo ambaye
alitamani sana baadaye awe mumewe.
Mama Levina hakujua kilichoendelea kabisa. Ilibaki kuwa siri ya Levina peke
yake.
Levina aliumia ndani
kwa ndani, alikiri kabisa kwamba Rashid hakuwa anahusika na chochote katika
mchezo ule. Kitu pekee kilichomsukuma kufanya vile ni mapenzi yake ya dhati
pekee, hakuwa na kitu kingine ndani yake zaidi ya hivyo.
Tangu Rashid
alipoondoka kwenda chumbani kwake kukusanya mizigo yake, alijisikia mkosaji
sana.
Mwenye roho mbaya
sana!
Alijihisi kama si
binadamu kabisa!
Sifa zote mbaya
akajipa yeye!
Mama yake aliweza
kugundua tofauti aliyokuwa nayo mwanaye, akaona njia pekee ya kugundua kilichokuwa
kikimtatiza mwanaye ni kumuuliza tu!
“Nini tatizo tena
mwanangu?”
Levina akabaki kimya!
“Levina...” mama yake
akaita.
“Abee...” Levina
akaitikia kwa kushtuka kidogo.
Ni kama alikuwa
amegutuka kutoka katika usingizi mzito, lakini ukweli haukuwa huo. Levina
alikuwa na mawazo ya usaliti. Kusema uongo na kumnyanyasa Rashid kwasababu ya
mapenzi.
“Una nini mama?!!”
“Inaniuma sana
mama...” Levina akasema machozi yakidondoka machoni mwake, ni kama alikuwa
akiumizwa na meseji za Rashid, lakini ukweli halisi haukuwa huo.
Ndani ya nafsi yake
alikuwa akiumizwa na kitendo cha kumsingizia na si kufanyiwa kama ambavyo
alitaka kutengeneza.
“Lakini ndiyo
nimemtimua hivyo.”
“Amekosa adabu kabisa,
yaani siku zote hizo naishi naye kama kaka yangu halafu anakuja kuniambia maneno
machafu kiasi hicho? Hana adabu kabisa...” akasema Levina lakini kichwani mwake
kukiwa na kitu kingine.
Moyoni mwake
alihifadhi kitu tofauti kabisa, alikuwa na siri nzito sana, ambayo hakutakiwa
kumwambia mtu yeyote, ilikuwa ni siri ambayo alitakiwa kuijua yeye na moyo wake
pekee.
“Potelea mbali, kama
ni kazi anaweza kupata mahali pengine, lakini nitapata wapi mwanaume kama Deo,
lazima nifanye hivi, sina namna!” akazidi kuwaza kichani mwake.
“Usijali mwanangu,
nimeshamtimua huyu mwanaharamu. Hutakiwi kuwa na mawazo mwanangu na mimi mama
yako nipo. Tena subiri...wewe Rashid, unasubiri nini? Kwani una mizigo gani
mingi ya kuchukua muda mrefu kiasi hicho?” akasema mama Levina akisimama
kumfuata chumbani kwake.
Mama Levina alikuwa
amevimba kwa hasira, akafika chumbani kwa Rashid na kumwita kwa sauti kubwa...
“Si naongea na wewe,
hebu toka haraka nyumbani kwangu.”
“Natoka mama, lakini
siku moja utakuja kugundua ukweli, siwezi kufanya mambo ya ujinga kiasi hicho
mama, kwakuwa wewe umeamua kumuamini
Levina sawa!”
“Tena funga domo lako
kabisa wewe mwanaharamu, inaonekana unataka kunigombanisha na mwanangu, unataka
kuniambia mwanangu anaongopa?”
“Ndiyo mama!”
“Kwa lipi hasa?”
“Sijui mama, lakini
ukichunguza utagundua ukweli.”
“Tena ishia hapo hapo
kuniita mama, anayeruhusiwa kuniita mama ni yule anayeheshimu wanangu na
kuwachukulia kama dada zake, si wewe mpumbavu!”
“Hapana mama!”
“We’ mwendawazimu,
sina muda wa kubishana zaidi. Paki vitu vyako, nakwenda kukuchukulia pesa zako
uondoke!”
Rashid akabaki kimya.
Mama Levina akaenda
ndani haraka na kuchukua fedha alizokuwa akidaiwa na Rashid kisha akarudi na
kumkuta tayari ameshajiandaa.
“Chukua pesa zako,
tena nimekuongezea na elfu thelathini zikusaidie, ondoka kwangu!”
“Ahsante mama, lakini
Mungu mwenyewe ndiye anayejua ukweli wa haya yote!”
“Hayo mahubiri yako
huwa nakutana nayo kanisani, sasa sioni kama hata hapa nyumbani kwangu panafaa
kuhubiriwa!”
“Siyo mahubiri mama,
ni ukweli kabisa kutoka ndani ya moyo wangu!”
“Ukweli wa nini?”
“Sijamtumia zile
meseji mimi mama.”
“Hivi wewe una akili?
Zile namba ni zako au za nani?”
“Zangu.”
“Sasa kama ni zako,
kwanini unaruka?”
“Unajua
mama...juzi...” mama Levina hakumpa nafasi ya kumalizia utetezi wake.
“Hebu toka kwangu
haraka tafadhali, sidhani kama bado nina nafasi ya kuendelea kuusikiliza utumbo
wako, ondoka tafadhali!”
Rashid alikuwa anataka
kumweleza mama Levina kwamba kuna siku alimuazima simu yake, lakini hakupewa
nafasi hiyo. Rashid akaondoka analia, mama Levina akiendelea kufoka huku
akirusha mikono.
Alikuwa amekasirika
sana. Pamoja na utendaji kazi wake kuwa mzuri kwa muda mrefu aliokuwa akikaa
naye, lakini siku aliyasahau yote hayo kwa meseji iliyoonekana kutumiwa
mwanaye.
***
Mto wote ulikuwa
umelowana kwa machozi, Levina alikuwa na uchungu sana ndani ya moyo wake. Usiku
huo ulikuwa mgumu sana kwake, aliteswa na watu mawili; DEO na RASHID!
Alifanya dhambi ya
kumsingizia Rashid kwamba amemtongoza na akafukuzwa kazi. Hilo lilimuuma,
lakini lingepoa kama kweli Deo angekubali kuwa naye. Lakini aliteseka sana,
akiwa hana uhakika kama kweli Deo atamkubalia.
Tabu yote ya nini?
Usiku ule ule akachukua simu na kumpigia Deo.
Itaendelea...